Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi

NEC Logo

Tume yamtangaza Bw.Khamis Yussuf Mussa kuwa mshindi wa Kiti cha Ubunge katika Jimbo la Kwahani

Imewekwa: 09 Jun, 2024
Tume yamtangaza Bw.Khamis Yussuf Mussa kuwa mshindi wa Kiti cha Ubunge katika Jimbo la Kwahani

Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) kupitia Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Kwahani-Zanzibar Bi.Safia Iddi Muhammad imemtangaza Bw.Khamis Yussuf Mussa kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwa mshindi wa Kiti cha Ubunge katika Jimbo la Kwahani.

Mussa almaarufu Pele ameibuka mshindi wa kiti hicho baada ya kupata Kura 7,092 Kati ya Kura halali 7,383 zilizopigwa na kuwabwaga wagombea wenzake 13 waliokuwa wakichuana katika uchaguzi mdogo wa jimbo hilo uliofanyika leo tarehe 8 Juni, 2024.

Jimbo la Kwahani lilikuwa na wapiga kura 11,936 na waliojitokeza kupiga kura ni 7,522 ambapo kura 139 zilikataliwa hivyo kufanya kura halali zilizopigwa kuwa ni 7,383.

Vyama 14 vilisimamisha wagombea katika Uchaguzi huo mdogo wa kiti cha Ubunge jimbo la Kwahani lililopo Wilaya ya Mjini Mkoa wa Mjini Magharibi.

Wagombea wengine na kura walizopata katika mabano ni pamoja na Bi. Jarade Ased Khamis  wa AAFP (06), Bi. Madina Mwalim Hamad wa ADA TADEA (49), Bi. Shara Amran Khamis  wa ADC (83), Bi. Zainab Maulid Abdallah  wa CCK (21), Bw. Abdi Khamis Ramadhan wa CUF(79), Bw.  Bashir Yatabu Said  wa Demokrasia Makaini (14) na Bi. Nuru Abdulla Shamte  wa DP(07) .

Wengine ni Bw. Kombo Ali Juma  wa NRA (05), Bi. Mwanakombo Hamad Hassan  wa NLD (08),  Bw. Amour Haji Ali  wa SAU(07), Bi. Naima Salum Hamad  wa UDP(01), Bi. Mashavu Alawi Haji  wa UMD(05) na Bi. Tatu Omary Mungi  wa UPDP(06).

Uchaguzi katika Jimbo la Kwahani umefanyika kufuatia kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), Ahmed Yahya Abdulwakil (65) kufariki dunia mwezi Aprili mwaka huu.